Musoma. Jeshi la Polisi mkoani Mara linawashikilia walimu wawili wa shule za msingi wilayani Butiama kwa tuhuma za kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanafunzi wa kidato cha pili.
Akizungumza leo Jumanne Machi 10, 2020 Kamanda wa Polisi mkoa wa Mara, Daniel Shillah amesema walimu wanadaiwa kushirikiana kumtorosha binti huyo mwenye umri wa miaka 19 aliyekuwa akisoma shule ya Sekondari Kukirango.
Amewataja walimu hao kuwa ni Kelvin Mwita (32) ambaye ni mwalimu wa shule ya Msingi Kiabakari A anayedaiwa kuwa na uhusiano na mwanafunzi huyo tangu akiwa shule ya msingi.
Amesema mwalimu mwingine ni Robert Msoke (28) wa shule ya Msingi Pida anayedaiwa kuishi na mwanafunzi huyo nyumbani kwake baada ya kumtorosha kwao akishirikiana na Mwita.
Amesema baada ya kufanya uchunguzi wa awali wamebaini kuwa Mwita alikuwa na uhusiano na binti huyo tangu akiwa anasoma shule ya msingi, waliendelea baada ya kuhitimu elimu ya msingi.
“Tumegundua huyo Msoke alikuwa na uhusiano na huyu mwanafunzi muda mrefu na uongozi wa kata ya Kukirango uliwahi kumuita na kumkanya juu ya tabia hiyo lakini naona alikaidi na kuendelea," amesema Shilla.
Pia Soma
- Majaliwa ahoji aliyemhamisha kuendelea na kazi
- Lema ahamasisha uchangiaji fedha viongozi Chadema wakikutwa na hatia
- MPYA: Mbowe wenzake wakutwa na hatia Kisutu
Amesema polisi wanaendelea na upelelezi, utakapokamilika hatua za kisheria zitachukuliwa.