Jeshi la Polisi linamshikilia Humphrey Humphrey (17), Mwanafunzi wa kidato cha tano, Shule ya Sekondari Iduda jijini Mbeya kwa tuhuma za mauaji ya Faraja Kasole (16) kwa kumkata na shoka kichwani baada ya kushindwa jaribio la kumbaka.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Urilich Matei ameliambia Mwananchi Digital leo Jumanne Septemba 6, 2022, tukio hilo limetokea Septemba 4, 2022 na kwamba marehemu alikuwa mwanafunzi kidato cha nne Shule ya Sekondari Sinde.
Matei amesema mtuhumiwa kabla ya kutekeleza mauaji hayo alifika nyumbani kwa marehemu anakoishi na wazazi wake, Kata ya Iganzo jijini Mbeya na kumkuta akiwa ndani peke yake ndipo alipomvamia na kutaka kumwingilia kimwili
''Baada ya purukushani na marehemu kumzidi nguvu mtuhumiwa ndipo alipochukua shoka lililokuwepo katika nyumba hiyo na kisha kumkata kichwani na kusababisha kifo chake baada ya kuvuja damu nyingi,'' amesema.
Amesema mtuhumiwa alipohojiwa na Polisi amekiri kuhusiana na tukio hilo na atafikishwa mahakamani mara baada ya uchunguzi kukamilika.