Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro linamshikilia mwanafunzi wa kidato cha pili (miaka 17) kwa tuhuma za kumuua rafiki yake, John Lema (18) chanzo kikielezwa kuwa, mabishano ya umri.
Mwanafunzi huyo mkazi wa Mtaa wa Kalimani, Wilaya ya Moshi inadaiwa yeye na Lema walikuwa marafiki na siku ya tukio walikaa kijiweni wakivuta sigara, wakaanza kubishana kuhusu umri kwamba nani mkubwa kati yao.
Inadaiwa kuwa, Lema alidai yeye ndiye mkubwa, jambo ambalo halikumfurahisha mwenzake aliyekuwa akidai ndiye mkubwa.
Inadaiwa baada ya mwanafunzi huyo kuona Lema anang’ang’ania ukubwa, aliamua kumshambulia kwa kumkata shingoni na mkononi kwa panga na kusababisha kifo chake.
Akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi Septemba 12, 2024, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa amesema tukio hilo lilitokea Jumatatu Septemba 9, mwaka huu, saa nne usiku, katika Mtaa wa Kalimani, eneo la Dampo, Kata ya Kaloleni, Wilaya ya Moshi.
*Pichani ni John Lema enzi za uhai wake