Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mwalimu kizimbani hasara ya milioni 11/-

6898 Mahakamanii TZW

Mon, 23 Apr 2018 Chanzo: habarileo.co.tz

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) wilayani Maswa mkoa wa Simiyu imemkamata na kumfikisha katika mahakama ya wilaya hiyo Mwalimu Josiha Mkome kwa kosa la kuisababishia serikali hasara ya Sh milioni 11.

Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Albetina Mwigira ameiambia mahakama hiyo kuwa mshitakwa alitenda kosa hilo kati ya Februari 2012 na Julai 2015 kinyume na kifungu namba 157 (1) na kinyume na kifungu 60 (2) cha sheria ya uhujumu uchumi kama ilivyo katika jedwali la 10 (1) la sheria hiyo.

Amesema mshitakiwa alikuwa ni mwalimu mwajiriwa wa Shule ya Msingi Shishiyu wilayani Maswa mkoani humo, kwa daraja la tatu la ualimu.

Mwigira amesema, akiwa katika kituo chake cha kazi, aliondoka kwa madai kuwa anaenda masomoni kujiendeleza kielimu na baada ya kutoka masomoni alielekea wilayani Magu alikoomba kuajiriwa.

Aliongeza akiwa wilayani Magu aliajiriwa na Halmashauri ya wilaya hiyo kufundisha Shule ya Sekondari Kandawe bila kutoa taarifa zozote kwa mwajiri wake ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa.

Mwigira alisema kwa muda wote huo mtuhumiwa alikuwa akichukua mshahara wake kupitia kwenye akaunti yake ya tawi la benki ya NMB Maswa huku akiwa hayuko kazini wala hafanyi kazi yoyote kwa mwajiri wake.

Alipopewa nafasi ya kujitetea mshitakiwa alikana shitaka na kupelekwa mahabusu baada ya kushindwa kukidhi masharti ya dhamana ambayo yalimtaka aweke dhamana Sh milioni sita au mali isiyohamishika yenye thamani sawa na fedha hiyo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama ya wilaya hiyo, Fredrick Lukuna ameahirisha kesi hiyo hadi kesho Aprili 24.

Chanzo: habarileo.co.tz