Mwanza. Justine Ogigo, mwalimu wa Shule ya Sekondari Itirio Wilaya ya Tarime mkoani Mara ameuawa kwa kuchomwa mkuki shingoni akiwa njiani kwenda kusimamia mitihani ya kidato cha pili inayoendelea nchini Tanzania.
Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu leo Alhamisi Novemba 14, 2019 mkuu wa Wilaya ya Tarime, Mtemi Msafiri amesema, “amechomwa mkuki alipofika eneo la Nyamongo.”
“Polisi wanawashikilia watu wanne kwa mahojiano kuhusu tukio hilo. Nitakuwa kwenye nafasi nzuri kuzungumzia suala hilo kiundani baada ya kufika msibani maana niko njiani kwenda Itirio kwenye msiba,” amesema Msafiri
Akizungumza kwa sharti la kuhifadhiwa jina mkazi wa Nyamongo amelieleza Mwananchi kuwa mwalimu huyo ameuawa kumetokana na kutozingatia mila na desturi inayokataza mtu kukatiza mbele ya vijana wanaotoka jandoni.
“Yawezekana hakufahamu masharti hayo ya kimila au alikuwa na haraka ya kuwahi kazini akadhani kwa sababu alikuwa akitumia usafiri wa pikipiki asingepata madhara,” amesema.