Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mwalimu Mkuu kikaangoni udanganyifu wa mitihani

C05b9ee6789dfea6770000f6366f8a00 Mwalimu Mkuu kikaangoni udanganyifu wa mitihani

Sat, 17 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Manyara imesema inasubiri mamlaka ya nidhamu mkoani humo imemchukulie hatua za kinidhamu Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Olkitikiti wilayani Kiteto, Oscar Waluye kabla ya kumfi kisha mahakamani kwa tuhuma za udanganyifu wakati wa mtihani ya darasa la saba.

Gazeti hili liliripoti Oktoba 9, mwaka huu kuwa Takukuru inamshikilia Waluye kwa kufanya udanganyifu katika mtihani huo kwa kuwalazimisha wanafunzi wawili wa darasa la sita shuleni hapo kufanya mtihani wa darasa la saba badala ya watahiniwa ambao uwezo wao darasani ulikuwa mdogo pamoja na kumkaririsha mwanafunzi mmoja.

Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Manyara, Holle Makungu alilieleza gazeti hili kwa njia ya simu kuwa Waluye hajafikishwa mahakamani na uchunguzi unaendelea kwa kuwa mtuhumiwa anakabiliwa na makosa ya jinai na kinadhamu kwani ni mtumishi wa umma.

Makungu alisema mamlaka ya nidhamu haijatoa uamuzi ingawa imeshaanza mchakato ukiwemo kumfuta kazi ili Takukuru iweze kumfikisha mahakamani mwalimu huyo.

“Tukimpeleka mahakamani kabla ya mamlaka ya nidhamu haijamfukuza kazi maana yake ni kwamba mamlaka hiyo haitaweza tena kumfukuza kazi mpaka kesi yake iishe na wakati huo huo mtuhumiwa ataendelea kupata mshahara, tukifanya hivyo tutakuwa tunaiingizia serikali hasara,” alisema.

Makungu alisema mtuhumiwa yuko nje kwa dhamana na atafikishwa mahakamani wakati wowote mamlaka ya nidhamu itakapokamilisha kazi yake, lakini pia uchunguzi utakapokamilika.

Kuhusu watoto waliolazimishwa kufanya mitihani hiyo, alisema Takukuru haioni sababu ya kuwashtaki kwa sababu walilazimishwa na mwalimu huyo kufanya mitihani hiyo na hata mwanafunzi aliyekaririshwa kwa kutumia jina la mwanafunzi mtoro, pia wataangaliwa cha kufanya kwa kuwa naye pia alifanya hivyo kwa maelekezo ya mwalimu.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kiteto, Tamim Kambona alisema tayari mwalimu huyo ameshachukuliwa hatua ya kinidhamu kwa kupewa barua ya kusimamishwa kazi na Idara ya Utumishi wa Walimu kwa mujibu wa taratibu, kanuni na sheria za mitihani.

Kambona alisema baada ya kumsimamisha kazi, wataendelea na vikao vya kinidhamu ambavyo vitamhukumu kwa mujibu wa sheria za mitihani kwa sababu alishakula kiapo cha usimamizi wa mitihani.

“Kwa hiyo hukumu yake itakuja kutoka lakini wakati wote huu atakuwa bado amesimamishwa kazi; kwa hiyo hukumu yake itakapotoka kama ni kufukuzwa kazi na utumishi atafukuzwa kazi na utumishi au kama ni kufukuzwa kazi tu basi atafukuzwa kazi au kama itaonekana afukuzwe kazi na ashitakiwe mahakamani, basi atafukuzwa na ataenda huko mahakamani, na kama ataonekana hana hatia atarudishwa kazini,” alisema Kambona.

Alisema hukumu yake itatoka baada ya vikao vya kinidhamu kukaa mwezi ujao au Desemba, lakini baada ya kusikiliza utetezi wake na endapo hataridhika na hukumu itakayotolewa anaweza kukata rufaa makao makuu

Chanzo: habarileo.co.tz