Tabora. Mkazi wa wilaya ya Bukombe mkoani Geita, Selemani Mashauri (37) anadaiwa kumuua kwa kumnyonga mkewe, Teddy Maro akimtuhumu kumwambukiza Virusi vya Ukimwi (VVU).
Baada ya kutekeleza mauji hayo, Mashauri naye anadaiwa kujiua kwa kujinyonga huku akiacha ujumbe unaoelezea sababu za vifo hivyo vilivyotokea mjini Igunga ambako wana ndoa hao walienda kutembelea ndugu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Emmanuel Nley jana alisema matukio hayo yalitokea Desemba 29, 2018 katika mtaa wa Hanihani mjini Igunga.
“Baada ya kumuua mkewe Teddy, Mashauri aliuficha mwili wake uvunguni mwa kitanda kabla naye kuchukua uamuzi wa kujinyonga akitumia mkanda wake wa suruali,” alisema. Mmoja wa majirani ambaye hakutaka kutajwa jina alisema pamoja na ujumbe ulioachwa na Mashauri kutaja kuambukizwa VVU kuwa chanzo cha mauaji hayo, inadaiwa kuwa maongezi ya simu aliyokuwa akifanya marehemu Teddy pia yalichangia kwani hayakumfurahisha mumewe aliyesikika akimtuhumu kuwa si mwaminifu.