Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Muharami, wenzake wazidi kusota rumande

Muharami Cambiasso We Muharami, wenzake wazidi kusota rumande

Wed, 29 Nov 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Aliyekuwa kocha wa makipa wa timu Simba, Muharami Sultani (40) na wenzake watano; wanaendea kusota rumande kutokana na upelelezi wa kesi inayowakabili kutokukamilika.

Sultan na wenzake watano wanakabiliwa na mashtaka manane yakiwemo ya kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroine kilo 34.89 na kutakatisha fedha.

Leo, Novemba 28, 2023 Wakili wa Serikali Frank Michael ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika hivyo anaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.

Wakili Michael, alitoa maelezo hayo, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Yusto Ruboroga, wakati kesi hiyo ilipoitwa kwa ajili ya kutajwa.

Kutokana na maelezo hayo, hakimu Ruboroga aliahirisha kesi hiyo hadi Desemba 11, 2023 itakapotajwa na washtakiwa wapo rumande kutokana na kesi ya kusafirisha dawa za kulevya na kutakatisha fedha kutokuwa na dhamana kwa mujibu wa sheria.

Kesi hiyo ilisikilizwa kwa njia ya video huku washtakiwa wakiwa rumande.

Mbali na Sultani, washtakiwa wengine ni mmiliki wa kituo cha Cambiasso Sport Academy kilichopo Tuangoma, Kambi Zubery Seif, Said Matwiko mkazi Magole, Maulid Mzungu maarufu mbonde, mkazi wa kisemvule ambaye ana uhusiano na mtuhumiwa Muharami, John John maarufu Chipanda, mkazi wa Kitunda ambaye kazi yake ilikuwa ni kutafuta vijana wenye vipaji na kuwapeleka Cambiasso Sport Academy, pamoja na Sarah Joseph.

Awali washtakiwa hao walikuwa wanakabiliwa na mashtaka matano lakini Septemba 23, 2023 Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP) aliwabadilishia hati ya mashtaka kwa kuwaongezea mashtaka matatu likiwemo la kutakatisha fedha na kisha kuwasomea upya mashtaka yao.

Katika shtaka la kwanza ni kuongoza genge la uhalifu ambalo linawakabili watu wote na inadaiwa tarehe tofauti kati ya mwaka 2016 na Novemba 4, 2022 maeneo tofauti na ndani ya Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani washtakiwa hao waliongoza genge la uhalifu kwa lengo la kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin Hydrochloride.

Shtaka la pili inadaiwa kuwa Oktoba 27, 2022 katika eneo la Kivule Wilaya ya Ilala mkoani Dar es Salaam washtakiwa hao kwa pamoja walikutwa wakisafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin zenye uzito wa kilo 27.10.

Shtaka la tatu inadaiwa kuwa Novemba 4, 2023 washtakiwa, Zuberi, Zungu na Mtwiko katika eneo la Kamegele Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani, walikutwa wakisafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin zenye uzito wa Kilo 7.79.

Katika shtaka la nne, tano, sita na saba ambayo ni ya utakatishaji fedha yanayomkabili mshtakiwa Kambi inadaiwa kuwa Aprili 15, 2021 katika Wilaya ya Ilala mkoani Dar es Salaam alinunua magari manne aina ya TATA yenye jina la Safia Group of Companies LTD huku akijua mali hizo zilipatikana kwa kosa la kuongoza genge la uhalifu.

Katika shtaka la nane inadaiwa kuwa Aprili 20, 2021 mshtakiwa Kambi alinunua gari aina ya TATA lenye jina Safia Group of Companies LTD akijua mali hiyo ilipatikana kwa kosa la kuongoza genge la uhalifu.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live