Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imeshindwa kusikiliza ushahidi katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili, Yusuf Ali Yusuf, maarufu ‘Mpemba wa Magufuli’.
Kesi hiyo imeshindwa kuanza kusikilizwa ushahidi kwa kile kilichoelezwa na upande wa mashtaka mtunza vielelezo katika kesi hiyo ni mgonjwa.
Yusuf na wenzake watano, wanakabiliwa na mashtaka manne ya kujihusisha na biashara haramu ya meno ya tembo yenye thamani ya Sh 785.6milioni, katika kesi ya Uhujumu Uchumi namba 53/2016.
Wakili wa Serikali Salimu Msemo akisaidiana na Candid Nasua ameieleza mahakama hiyo, leo Alhamisi Juni 27, 2019, wakati shauri hilo lilipofikishwa mahakamani hapo wa ajili ya ushahidi.
Msemo amedai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba kuwa, amepewa taarifa asubuhi kuwa anayetunza vielelezo katika kesi hiyo, ambavyo ni meno ya tembo ni mgonjwa hali ilipelekea ashindwe kufika ofisini kwake.
" Licha ya mtunza vielelezo kuwa mgonjwa, upande wa mashtaka tunaye shahidi aitwaye Daniel Gumbo, ambaye ni ofisa kutoka Maliasili, hivyo tunaomba mahakama yako imuombe ili tarehe ijayo aweze kuhudhuria katika kesi hii" alidai wakili Msemo na kuongeza kuwa
Pia Soma
- Zitto ataka Bunge kuibana Serikali ya Tanzania kuhusu kukopa
- Tiba asili za barabarani zapigwa marufuku Iringa
- Nyama ya nyumbu yampandisha kortini mtumishi wa hifadhi ya Ikona
- Kiongozi wa mbio za Mwenge amgomea Mkuu wa Wilaya ya Mwanga
"Kutokana na hali hiyo, tunaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kuanza kusikiliza ushahidi" alidai Msemo.
Hakimu Simba baada ya kusikiliza hoja hizo, amesema kesi hiyo ni ya muda mrefu hivyo amepanga kuisikiliza kesi hiyo kwa siku tatu mfululizo kuanzia Julai 11, 18 na 24.
Baada ya kueleza hayo, hakimu Simba ameahirisha kesi hiyo na washtakiwa wamerudishwa rumande kutokana na mashtaka yanayowakabili kutokuwa na dhamana.
Mbali na Yusuph(35), washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Charles Mrutu(37), maarufu kama mangi mapikipiki na mkazi wa Mlimba, Morogoro; Benedict Kungwa(40), mkazi wa Mbagala Chamazi; Jumanne Chima(30), maarufu kama JK na mkazi wa Mbezi; Ahmed Nyagongo(33), dereva na mkazi wa Vikindu-Mkuranga na Pius Kulagwa(46)mfanyabiashara na mkazi wa Temeke.
Moja kati ya mashtaka yanayowakabili washtakiwa hao ni kwamba, kati ya Januari, 2014 na Oktoba, 2016, katika maeneo ya Jiji la Dar es Salaam, Tanga, Iringa na Mtwara, washtakiwa kwa pamoja walijihusisha na mtandao wa ujangili kwa kukusanya na kuuza nyara za Serikali ambazo ni vipande 50 vya meno ya tembo vyenye thamani ya dola za Marekani 180,000 sawa na Sh392,817,600 bila kuwa na kibali cha Mkurugenzi wa Wanyamapori.