MTOTO Juma Megejuwa (12) mkazi wa Kijiji cha Mwaningi katika Kata ya Bulige wilayani Kahama mkoani Shinyanga, amefariki dunia baada ya kunywa dawa ya kienyeji kwa mzazi wake ambaye ni mganga wa kienyeji kwa lengo la kusafishwa nyota.
Aidha, watu wawili ambao ni ndugu, Loya Ngusa (66) na Bahati Ngusa (25) nao baada ya kunywa dawa hiyo, walizirai na kukimbizwa katika kituo cha afya kupatiwa matibabu.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Debora Magiligimba, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo nyumbani kwa mganga huyo aliyefahamika kwa jina la Dela Megejuwa (44).
Magiligimba alisema mtoto huyo alifariki dunia juzi saa tisa alasiri, na kwamba, wateja wengine wawili wa mganga huyo waliokwenda kutibiwa ili kusafisha nyota akiwemo jirani wa mganga huyo na mwingine mkazi wa Shilima, Kwimba mkoani Mwanza, walizirai.