Jeshi la polisi Mkoa wa Simiyu linamshikilia kinara wa kutengeneza magobole, risasi na makasha ya risasi 34.
Katika taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Simiyu, Blasius Chatanda leo Jumamosi Agosti 20, 2022 wilayani Bariadi mkoani hapa imeeleza kuwa jeshi la polisi kupitia kikosi kazi maalumu liliendesha oparesheni ya ukamataji wa silaha zinazomilikiwa kinyume cha sheria.
Katika msako huo wamefanikiwa kukamata watuhumiwa sita pamoja na fundi anayedaiwa kujihusisha na utengenezaji wa magobore na kuwauzia watu mbalimbali.
Amesema katika uchunguzi wa kina walioufanya wamebaini kuwa baadhi ya silaha zilizotengenezwa kienyeji zimekuwa zikitumika katika matukio ya uhalifu kwenye mikoa ya Kanda ya Ziwa.
"Silaha hizo zimekuwa zikitumika katika matukio ya ujangili katika maeneo ya Hifadhi Serengeti na pori la akiba la wanyamapori Maswa, watuhumiwa wengine watano walivyohojiwa walikiri kumiliki silaha hizo bila kuwa na vibali," amesema
Amesema baadhi ya silaha hizo zinatumika shughuli za ulinzi wa kampuni binafsi maeneo ya Simiyu, Shinyanga, Kahama na Mwanza.
Amebainisha kuwa oparesheni hiyo ni endelevu kwa lengo la kudhibiti umiliki holela wa silaha katika jamii na watuhumiwa wote watafikishwa mahakamani haraka iwezekanavyo.