Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Msudani aliyekamatwa na dola 60,000 JNIA apandishwa kizimbani

22442 RAIA+PIC TanzaniaWeb

Tue, 16 Oct 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Raia  wa Sudan, Nada Zaelnoon Ahmed Elbokhary (38) leo Oktoba 15, 2018 amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kujibu shtaka la kukutwa na dola za kimarekani 60,000 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl Julius Nyerere (JNIA) ambazo hajazitolea taarifa kwa mamlaka husika.

Elbokhary ambaye ni mkazi wa Masaki jijini,  ametakiwa, kujibu shtaka moja la kushindwa kutolea taarifa ya fedha hizo kwa Mamlaka ya Forodha.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Patrick Mwita amedai, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, kuwa mshtakiwa ametenda kosa hilo Oktoba 9, 2018 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere uliopo katika wilaya ya Ilala jijini.

Mwita amesema siku hiyo, mshtakiwa Elbokhary wakati akiondoka Tanzania kuelekea Sudan, alikutwa akiwa na dola za Marekani 60,000 ambazo ni zaidi ya Sh.120 milioni na paundi 3,410 za Sudan ambazo hakuzitolea maelezo kwa mamlaka ya forodha.

Mshtakiwa amekana kutenda kosa hilo na upande wa mashtaka umedai kuwa upelelezi wa shauri hilo umekamilika.

Hakimu Simba ametoa masharti ya dhamana ambayo ni kuwa  na wadhamini wawili wanaotambulika kisheria watakaosaini bondi ya Sh 20 milioni kila mmoja.

Pia mahakama hiyo imemtaka mshtakiwa huyo kuwasilisha hati yake ya kusafiria mahakamani hapo.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Oktoba 22 Mwaka huu itakapokuja kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa maelezo ya awali (PH).

Mshtakiwa ameshindwa kutimiza masharti ya dhamana na kurudishwa rumande.

 

 

Chanzo: mwananchi.co.tz