Zanzibar. Msichana mwenye ulemavu wa akili (22) jina linahifadhiwa anadaiwa kufungiwa ndani kwa miaka minne.
Hayo yalielezwa jana katika kongamano la kupinga unyanyasaji kwa walemavu lililoandaliwa na Jumuiya ya wenye ulemavu wa akili Pemba (ZAPDD).
Katika kongamano hilo, wadau walielezwa msichana huyo ni mkazi wa wilaya ya Chakechake, Kusini Pemba na amefungwa minyororo na kuwekwa kwenye chumba chenye giza.
Mkuu wa Dawati la Jinsia kutoka Jeshi la Polisi Wilaya ya Chakechake, Zuwena Hamad Ali alisema mazingira ya chumba alichokuwamo binti huyo hayaridhishi kwa binadamu kuishi.
“Cha kusikitisha zaidi ndani ya chumba hicho pia kulikuwa na kuku. Hata afya yake imedhoofu sana kwa sababu ya kukaa ndani muda mrefu,” alisema Zuwena.
Mwenyekiti wa ZAPDD mkoa wa Kaskazini, Aziza Alawy Mussa alisema tukio la kufungiwa ndani binti huyo ni unyama na udhalilishaji mkubwa.
Hakimu wa Mahakama ya Mkoa Chakechake, Khamis Ali Simai aliishauri ZAPDD kushughulikia kwa haraka kesi za wenye ulemavu wa akili zinapofikishwa mahakamani ili hatua zichukuliwe haraka kukomesha vitendo hivyo.