Dar es Salaam. Mkazi wa mkoani Dodoma, Abdallah Bawaziri amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na kesi ya mauaji ya mwanaharakati wa kupambana na ujangili, Wayne Lotter.
Bawaziri amefikishwa mahakamani hapo leo Ijumaa Oktoba 25, 2029 na kuunganishwa na washtakiwa wengine 16 wanaokabiliwa na kesi hiyo.
Wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon amedai mshtakiwa anakabiliwa na mashtaka mawili ya kula njama na kumuua Lotter.
Simon amedai mbele ya Hakimu Mkazi mfawidhi, Kelvin Mhina kuwa mshtakiwa anadaiwa kutenda makosa hayo kati ya Julai Mosi na Agosti 16, 2017.
Katika shtaka la pili, Bawaziri anadaiwa Agosti 16, 2017 katika makutano ya barabara za Chole na Haile Selasie iliyopo wilaya ya Kinondoni, anadaiwa kumuua Lotter, mwanzilishi mwenza wa Shirika lisilo la kiserikali la Palms Foundation.
Mshtakiwa baada ya kusomewa mashtaka yanayomkabili hakutakiwa kujibu chochote kutokana na Mahakama hiyo kutokuwa na uwezo wa kusikiliza kesi za mauaji.
Pia Soma
- Wapandishwa kizimbani kwa madai ya kukutwa na tausi wa Ikulu
- Hamahama ya halmashauri vurugu tupu
- China yaunga mkono Zimbabwe kuondolewa vikwazo
Bawaziri na wenzake wamerudishwa rumande kutokana na kesi ya mauaji kutokuwa na dhamana kwa mujibu wa sheria.
Mbali na Bawaziri, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ya mauaji namba 19/2017 ni raia wawili wa Burundi, Nduimana Jonas na Bonimana Nyandwi.
Wengine ni Godfrey Salamba, Innocent Kimaro, Chambie Ally, Robert Mwaipyana, Khalid Mwinyi, Rahma Almas, Allan Mafue, Ismail Mohammed, Leornad Makoye, Amino Sham, Ayoub Selemani, Joseph Lukoa, Gaudence Matemu na Abuu Mkingie.