Arusha. Mkurugenzi wa Kampuni ya Ortello Business Cooperation (OBC) Isack Mollel leo Jumatatu Machi 4, 2019 amepandishwa kizimbani akikabiliwa na makosa 10 ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha.
Mbali ya Mollel pia kampuni ya OBC ambayo inamilikiwa na Falme za Kiarabu inashitakiwa kwa makosa ya utakatishaji fedha na kuisababishia Serikali hasara ya 2.8 bilioni.
Wakili Mkuu wa Serikali, Oswald Tibabyekomya, ameyasema wakati akimsomea mashitaka hayo, Mollel mbele ya hakimu mfawidhi wa mahakama ya mkoa Arusha, Liku Mwakatobe.
Hata hivyo, Mollel ambaye anatetewa na mawakili, Osward Kimomogoro, Daudi Haraka na Godluck Peter hakutakiwa kujibu lolote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo.
Kesi hiyo imeahirishwa hadiĀ Machi 18, 2019 na mtuhumiwa amepelekwa mahabusu Gereza Kuu la Kisongo, Arusha.