Watu watano wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza kwa tuhuma za mauaji ya Sophia Maduka (61) na Mathias Lusesa (73) ambao ni mke na mume wanaokaa Kijiji cha Lwenge, Kata ya Kagunga Wilaya ya Sengerema.
Kamanda wa Polisi mkoani humo Wilbroad Mutafungwa amesema tukio hilo limetokea Desemba 12, 2023 na watu hao wanadaiwa kuvamia nyumbani kwa wanandoa hao na kuwashambulia kwa mapanga hadi kufariki, kisha watu hao wakatokomea kusikojulikana.
Kamanda Mutafungwa amesema January 06, 2024 kupitia msako maalum uliofanywa na Jeshi hilo umewabaini watuhumiwa hao waliohusika na mauaji.
Kamanda huyo ameongeza kuwa baada ya kuwahoji watu hao wamesema chanzo cha mauaji waliyoyafanya ni Imani za Kishirikina, huku Kamanda Mutafungwa akisema pindi upelelezi utakapokamilika watafikishwa Mahakamani kwa ajili ya kuchukuliwa hatua za kisheria.