Tanga. Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Tanzania (DCEA) imemkamata Hamad Mbaraka kwa tuhuma za kukutwa na gramu 500 za dawa za kulevya aina ya Heroin.
Mtuhumiwa huyo mkazi wa barabara ya 19 Wilaya ya Tanga mjini amekamatwa usiku wa kuamkia leo Jumatatu Februari 17, 2020.
Akizungumza leo kaimu Kamishna Jenerali wa DCEA, James Kaji amesema mtuhumiwa huyo alikamatwa saa 6 usiku, “alikuwa amezificha katika mfuko mmoja wa plastiki ndani yake kulikuwa na pakiti tatu tofauti zilizokuwa na dawa hizo.”
“Tangu saa 2 usiku jana tulikuwa tunamtafuta mtuhumiwa, tulikuwa tunafanya mawasiliano ila ilipofika saa 6 usiku tulimkamata, kwa sasa yupo mahabusu anaendelea kuhojiwa.”
Amesema wamepeleka kithibitisho hicho kwa mkemia mkuu wa Serikali kwa ajili ya kupimwa.
Amebainisha kuwa katika mahojiano mtuhumiwa huyo amekiri kuwa anapopatiwa dawa hizo huzificha kwenye mashamba eneo la Pangani.