Serengeti. Mahakama ya hakimu mkazi mfawidhi Wilaya ya Serengeti Mkoa wa Mara imewahukumu kifungo cha miaka 20 jela washtakiwa wawili wa kesi za uhujumu uchumi.
Waliohukumiwa ni Amosi Sarya na David Mahanga, wakazi wa kijiji cha Kibeyo wilayani Serengeti Mkoa wa Mara.
Akisoma hukumu hiyo leo Alhamisi Mei 30, 2019 hakimu Ismael Ngaile amesema mahakama imeridhishwa na ushahidi uliotolewa na upande wa Jamhuri na kubainisha kuwa kila mmoja atatumikia kifungo cha miaka 20 jela.
Awali, mwendesha mashtaka wa Serikali, Emmanuel Zumba amesema washtakiwa walikamatwa Juni Mosi, 2018 eneo la Samaki ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti wakiwa na ngozi mbili za nyumbu na nyamera zenye thamani ya zaidi Sh3.2 milioni.
Amesema washtakiwa hao pia walikutwa na mapanga mawili, kisu kimoja na nyaya nne za kutegea wanyama.
Amebainisha kuwa walifikishwa mahakamani kwa makosa matatu ya uhujumu ikiwa ni pamoja na kuingia ndani ya hifadhi, kukutwa na silaha na kukutwa na nyara za Serikali bila kibali.
Pia Soma
- Dk Abbas asema sekta ya madini Tanzania imeonyesha mwanga
- Katibu wa CCM Kunduchi kusomewa maelezo ya awali
- Nishati jadidifu ilivyobadili maisha kijiji cha Lukumbule