Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuachia huru mhasibu mkuu wa Bodi ya Pamba Tanzania (TCB), Simon Maganga baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) kuieleza mahakama hiyo kuwa hana nia ya kuendelea na kesi.
Maganga alikuwa anakabiliwa na mashtaka sita likiwemo la kuisababishia Serikali hasara ya ShSh55.6 milioni.
Mhasibu huyo amefutiwa kesi hiyo chini ya kifungu namba 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ( CPA) sura ya 20 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Maghela Ndimbo akisidiana na Nickson Shayo ameieleza mahakama hiyo leo Jumatano Julai 24, 2019 mbele ya hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya utajwa.
Ndimbo amedai DPP hana nia ya kuendelea na shauri hilo dhidi ya mshtakiwa kuomba kuiondoa mahakamani.
Hakimu Simba baada ya kusikiliza maelezo ya upande wa mashtaka, amesema analiondoa mahakamani kama upande wa mashtaka walivyoeleza.
Pia Soma
- Ilichokisema TIC kuhusu korosho
- Kampuni 30 hatarini kufutiwa leseni
- Sekondari Bwiru kutoa elimu ya ujasiriamali
Maganga anadaiwa Januari 2009 alimdanganya mwajiri wake kwa kutumia vocha za kuwasilisha mbegu za pamba katika msimu wa mwaka 2009/10 akijaribu kuonyesha kampuni ya Afrisian Ginning Limited ilinunua mbegu za pamba kilo 25.1milioni.
Pia, Maganga alifanya hivyo kwa kampuni ya Nyanza Cooperative Limited kwa kuonyesha kuwa ilinunua kilo 3.7milioni za mbegu za pamba wakati akijua siyo kweli.
Katika shtaka lingine, mshtakiwa anadaiwa kutumia vocha za kuwasilisha mbegu za pamba msimu wa 2009/10 akijaribu kuonyesha Kampuni ya S&C Ginning Limited ilinunua kilo 17.1milioni za mbegu za pamba.
Maganga akiwa kama mhasibu wa TCB, alifanya ufujaji na ubadhirifu wa fedha kiasi cha Sh55.6 milioni mali ya TCB.