Teaser title: Mhasibu Chuo cha Ustawi wa jamii atupwa jela miaka mitano
Summary: Ni baada ya kupatikana na hatia ya wizi ya zaidi ya Sh5milioni fedha za wanafunzi.
Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuhukumu kifungo cha miaka mitano jela aliyekuwa Mhasibu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii, Gryson Mnyawami baada ya kupatikana na hatia ya wizi wa zaidi ya Sh9 milioni akiwa mtumishi wa umma.
Hakimu Mkazi Mkuu, Janeth Mtega ametoa hukumu hiyo leo Agosti 16 baada ya kupitia ushahidi wa mashahidi watano wa upande wa mashtaka ambao walithibitisha wizi huo pasipo kuacha shaka.
Wakili wa Serikali Janeth Magoho ameieleza mahakama kuwa mshtakiwa huyo ni mkosaji wa kwanza na hakuna kumbukumbu za makosa mengine.
Hata hivyo, Magoho aliiomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mshtakiwa huyo kwa kuwa kitendo cha wizi alichofanya akiwa mtumishi wa umma ni kibaya na kinaitia hasara Serikali.
Ameongeza kuwa, suala la wizi katika Chuo cha ustawi limekuwa likitokea mara kwa mara.
“Kitendo hicho ni kudhulumu wanafunzi na kwamba siyo cha haki kwani ile fedha ni fedha ya walipa kodi hivyo adhabu kali itakuwa fundisho kwake na kwa wengine wenye tabia kama hiyo,”amesema
Mnyawami katika utetezi wake aliiomba mahakama hiyo kumpunguzia adhabu na alikubali kulipa fedha hizo taratibu lakini taasisi ndiyo ilimkatalia.
Ameongeza kuomba apunguziwe adhabu kwa kuwa dada yake ni mgonjwa na mama yake ni mjane na wote wanamtegemea yeye.
Baada ya kusikiliza hoja hizo Hakimu Mtega alimuhukumu mshtakiwa huyo kifungo cha miaka mitano jela.