MGANGA wa Kienyeji Mayala Hinyali (32) anashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Katavi kwa tuhuma za kumtorosha na kuishi naye kinyumba mwanafunzi wa kike mwenye umri wa miaka 16.
Msichana huyo anadaiwa kujiunga na kidato cha kwanza Januari mwaka huu katika Shule ya Sekondari ya Usevya iliyopo Halmashauri ya Mpimbwe Wilaya ya Mlele mkoani humo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Benjamini Kuzaga amethibitisha kukamatwa kwa mganga huyo wa kienyeji Machi 3, nyumbani kwake Kijiji cha Kasekese katika Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika.
Kamanda Kuzaga amesema wawili hao walikutwa wakiishi kinyumba kama mume na mke na kwamba mtuhumiwa huyo atafikishwa mahakamani ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia ya kukatisha ndoto za wasichana na wanaoendekeza ndoa za utotoni.