Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mfanyabiashara kizimbani kwa utakatishaji

Tapeli.jpeg Paul Msoka akiwa katika viunga vya Mahakama

Mon, 24 Jan 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mfanyabiashara Paul Msoka 47, anayeishi Ukonga Kichangani, amefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashitaka sita yakiwemo ya kugushi, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na utakatishaji wa USD 225,600. Katika hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo na wakili wa serikali Mwandamizi Jackline Nyantori mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Richard Kabate imedai kuwa, mshtakiwa anadaiwa kutenda makosa sita ya kughushi, kosa moja la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kutakatisha fedha.

Akisoma hati ya mashtaka, Nyantori amedai, Aprili 24 mwaka 2021 jijini Dar es Salaam mshtakiwa aligushi nyaraka ya Kampuniya ACGB International Trade ,LLC, United State of America (USA), akidai kuwa kampuni hizo zimeingia katika mkataba na Kampuni ya madini ya Tanganyika (Tanganyika Mining Company Ltd)ambayo ni kampuni ya kitanzania wa kuuza kilo 20 ya madini ya dhahabu na kusafirisha kwenda San Diego, California, Marekani wakati akijua si kweli.

Katika shtaka la pili imedaiwa, Desemba 13 mwaka jana, mshtakiwa Msoka kwa nia ovu na kwa udanganyifu aligushi cheti akionesha kuwa, kimetolewa na Baraza la Taifa la Biashara, viwanda na Kilimo kwamba limepitisha boksi la kilo 20 za madini ya dhahabu kwa ajili ya kusafirishwa na Kampuni ya Tanganyika Mining Company Ltd jambo ambalo limedhibitishwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) huku akijua si kweli.

Mshtakiwa pia anadaiwa kughush hati ya kubadili umiliki ya Desemba 13, akionesha Southern African Development Community (SADC) imetoa mabadiliko ya umiliki wa hati hiyo kuruhusu Kampuni ya Tanganyika Mining Company Ltd kusafirisha kilo 20 ya madini ya dhahabu na zisafirishwe kwenda ACGB International Trade iliyoko San Marcos, Marekani wakati akijua si kweli.

Aidha Msoka anadaiwa, Desemba 8 ,mwaka 2021 aligushi nyaraka zilizoonesha kwamba zimetolewa na Baraza la Usimamizi wa Amani la Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo (MONUSCO) na kwamba zilizotolewa kwa Kampuni ya Tanganyika Mining Company Ltd ya tanzania kuiruhusu Kampuni hiyo kusafirisha kilo 20 za dhahabu kutoka Kongo kwenda kwa Kampuni ya ACGB International Trade ya Marekani jambo ambalo alijua si kweli.

Katika shtaka la tano, imedaiwa kati ya Juni mosi mwaka 2021 na Januari 11 mwaka 2022 Msoka, kwa njia ya udanganyifu alijipatia kutoka kwa Aldo Costa ambaye ni mwakilishi wa ACGB International Trade,LLC, ya Marekani USD 225,600 akidanganya kwamba angesambaza kilo 20 ya dhahabu kwa Kampuni ya ACGB wakati akijua si kweli.

Katika shitaka la utakatishaji, inadaiwa, mshitakiwa alijipatia kiasi hicho cha fedha kutoka kwa Aldo Costa huku akijua fedha hizo ni mazalia ya makosa tangulizi ya kugushi.

Hata hivyo mshtakiwa hakuruhusiwa kujibu kitu chochote mahakamani hapo kwa kuwa mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi ambazo kwa kawaida husikilizwa Mahakama Kuu.

Kwa mujibu wa upande wa mashtaka upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika na kesi hiyo imeahirishwa hadi Februari 7, kwa ajili ya kuja kutajwa tena.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live