MAHAKAMA Kuu, Kitengo cha Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, imemhukumu kifungo cha miaka 30 jela mfanyabiashara maarufu jijini Tanga, Yanga Omary Yanga, maarufu kwa jina la “Rais wa Tanga kwa kusafirisha dawa za kulevya aina na herion zenye uzito wa gramu 1052.63.
Pia mahakama hiyo imewaachia huru washitakiwa wengine Rahma Juma, ambaye ni mke wa Yanga na Halima Mohamed, ambaye ni mfanyakazi wa ndani kwa kuwa ushahidi uliotolewa dhidi yao ulikuwa hafifu.
Hukumu hiyo ilisomwa na Jaji Imakulata Banzi katika Mahakama Kuu, Kanda ya Tanga, baada ya kumtia hatiani mfanyabiashara huyo kwa kwa kuzingatia ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka.
Alisema kuwa upande wa mashitaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu Faraja Nchimbi ulipitia ushahidi wa mashahidi saba na vielelezo kumi na kuthibitisha pasipo kuacha shaka yoyote kuwa Yanga alikuwa akijihusisha na biashara hiyo haramu ya dawa za kulevya.