Dar es Salaam. Upelelezi wa kesi ya kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin inayomkabili mfanyabiashara Hariri Mohamed Hariri bado haujakamilika, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeelezwa leo Jumatano Desemba 19, 2018.
Hariri anaendelea kusota rumande kwa takribani miezi tisa kutokana na upelelezi na kutokamilika kwa upelelezi wa shauri hilo.
Hariri alifikishwa Kisutu kwa mara ya kwanza Machi 20, 2018 kujibu shtaka moja la kusafirisha dawa za kulevya.
Leo wakili wa Serikali, Esther Martine ameieleza mahakama hiyo kuwa shauri hilo bado halijakamilika na kuomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.
Hakimu Mkazi Janeth Mtega baada ya kusikiliza maelezo ya upande wa mashtaka ameahirisha kesi hiyo hadi Januari 2, 2019 na mshtakiwa kurejeshwa rumande kutokana na shtaka linalomkabili kutokuwa na dhamana.
Katika kesi ya msingi, Hariri anadaiwa kutenda kosa hilo Machi 2, 2018 eneo la Kinondoni Matitu, Dar es Salaam.
Mshtakiwa anadaiwa siku hiyo alikutwa akisafirisha gramu 214.11 za dawa za kulevya aina ya Heroin.
Soma Zaidi: Kigogo dawa za kulevya apandishwa kizimbani