Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Meno ya tembo yapeleka wanne jela miaka 20 kila mmoja

Wed, 22 May 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imewahukumu watu wanne, kutumikia kifungo cha miaka 20 kila mmoja baada ya kupatikana na hatia ya kujihusisha na biashara haramu ya meno ya tembo yenye thamani ya Sh32.5 milioni.

 

Pia, Mahakama hiyo imeamuru kutaifishwa kwa gari lilotumika kubeba vipande sita vya meno ya tembo.

 

Washitakiwa katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 31/ 2016 ni Solomon Mtenya, Siasa Athumani, Musa Ligagabile na Omary Sabo.

 

Pia Soma

Akitoa hukumu hiyo leo Jumatano Mei 22, 2019, Hakimu Mkazi Mwandamizi, Maira Kasonde amesema Mahakama yake imewatia hatiani washtakiwa hao kama walivyoshtakiwa.

 

Akisoma hukumu hiyo, Kasonde alisema katika shtaka la kwanza la kujihusisha na genge la uhalifu, washtakiwa watatumikia kifungo cha miaka mitano jela bila faini.

“Katika shitaka la pili ambalo ni  kujihusisha na biashara haramu ya meno ya tembo, washtakiwa wote kwa pamoja watatumikia kifungo cha miaka miwili jela kila mmoja bila faini,” amesema Hakimu Kasonde.

 

Hakimu Kasonde alisema katika shtaka la tatu, ambalo ni kukutwa na vipande sita vya meno ya tembo ndani ya gari, washtakiwa wote watatumikia kifungo cha miaka 20 jela kila mmoja.

Alisema upande wa mashtaka ulipeleka mashahidi 11 ambao walithibitisha mashtaka pasina shaka.

“Kutokana na kitendo walichofanya washtakiwa hawa, mahakama hii inawahukumu kutumikia kifungo cha miaka 20 jela kila mmoja, ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia kama hii na kwamba, adhabu hiyo inakwenda kwa pamoja.

“Pia, gari aina ya Toyota Funcargo iliyotumika kubeba meno hayo ya tembo imetaifishwa na Serikali na haki ya kukata rufaa iko wazi kwa mtu ambaye hajaridhika na hukumu hii,” amesema hakimu huyo.

 

Awali, kabla ya kutolewa kwa hukumu, Wakili wa Serikali, Salimu Msemo akisaidiana na Constantine Kakula, aliiomba mahakama kutoa adhabu kali dhidi washtakiwa hao ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia kama hiyo.

Kwa mujibu ya hati ya mashtaka, washtakiwa wanakabiliwa na mashtaka matatu likiwamo la kukutwa na vipande vya meno ya tembo.

Na wanadaiwa kutenda makosa hayo Juni 23, 2016 eneo la Kimara.

 

Siku ya tukio, washtakiwa  walikutwa na vipande sita vya meno ya tembo vyenye thamani ya Dola za Marekani 15,000 sawa na Sh 32,565, 000 , bila kuwa na kibali kutoka kwa Mkurugenzi wa Wanyamapori nchini.

 

Chanzo: mwananchi.co.tz