Dar Es Salaam. Aliyekuwa Meneja wa Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) tawi la Mkwepu, Priscus Shirima (37) amefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kujibu mashtaka matatu likiwemo la kutakatisha fedha.
Shirima ambaye ni mfanyabaishara na mkazi wa Dodoma Area D amefikishwa leo Alhamisi Desemba 13, 2018 kujibu mashtaka hayo katika kesi ya uhujumu uchumi namba 95/2018.
Wakili wa Serikali, Wankyo Simon amedai mbele ya Hakimu Mfawidhi, Kelvin Mhina kuwa mshtakiwa anakabiliwa na mashtaka matatu ya kufanya miamala ya uongo akiwa mtumishi wa benki hiyo, wizi na kutakatisha fedha kiasi cha Sh120 milioni.
Simon amedai katika shtaka la kwanza la kufanya mwamala wa uongo akiwa ofisa wa benki, Shirima anadaiwa kuwa Juni 20, 2016 akiwa na nia uovu alifanya muamala wa uongo kwa kuhamisha Sh120milioni kutoka akaunti namba 0310137001 ya Florah Lyatuu kwenda akaunti yake namba 0380073121.
Katika shtaka la pili la wizi akiwa mtumishi, Shirima anadaiwa siku na eneo hilo aliiba Sh120 milioni.
Shtaka la tatu ambalo ni utakatishaji fedha, mshtakiwa anadaiwa kutenda kosa hilo kati ya Juni 2016 katika benki hiyo.
Anadaiwa alijihusisha na muamala wa Sh120milioni kwa kuruhusu na kufanya malipo kutoka akaunti namba 0380073121 inayomilikiwa na shirika, akilipa kampuni ya Sekorizi Ltd kupitia hundi tatu zenye namba 000127, 648806 na 1648791 huku akifahamu kuwa fedha hizo si halali.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo hakimu Mhina amesema hapaswi kusema chochote kutoka na Mahakama ya Kisutu kutokuwa na uwezo wa kusikiliza shauri hilo.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Desemba 27, 2018 itakapotajwa na mshtakiwa kurudishwa rumande.