MENEJA Ujenzi aliyekuwa akisimamia maendeleo ya ujenzi eneo jirani na reli ambapo treni ya abiria ya Taiwan ilipata ajali na kuua abiria 50, amekamatwa kwa mahojiano baada ya kuhusishwa kufanya uzembe ambapo lori mojawapo la ujenzi linadaiwa kugonga treni hiyo na kuisababisha iache njia yake na kupinduka.
Meneja huyo alikamatwa juzi na kuhojiwa kisha akaachiwa kwa dhamana wakati upelelezi ukiendelea.
Wakati huohuo waokoaji wanaendelea kupekua eneo la ajali kuona iwapo wanaweza kupata miili mingine iliyokwama ndani ya njia ya reli chini ya ardhi.
Treni hiyo ilikuwa inatoka Taipei kwenda Taitung na ilikuwa imepakia abiria zaidi ya 500 ambao wengi walikuwa ndugu wanaokwenda kusherekea sikukuu na familia zao.
Treni hiyo ilipofika eneo la Hualien na kuanza kupita kweye handaki ndipo ilipopata ajali na kusababisha vifo hivyo na abiria wengine kujeruhiwa.
Ajali hiyo ilitokea juzi asubuhi ambapo abiria 50 walikufa na majeruhi 66 baadhi yao wanaendelea na matibabu na abiria wengine wameokolewa.
Katika majeruhi hao, wanapatiwa matibabu katika hospitali sita tofauti za Kaunti ya Hualien.