Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mchunguzi Mkuu TAKUKURU aeleza alivyochunguza fedha za CWT

Cwtp Ic Mchunguzi Mkuu TAKUKURU aeleza alivyochunguza fedha za CWT

Wed, 20 Oct 2021 Chanzo: mwananchidigital

Mchunguzi Mkuu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Mercy Manyalika ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu alivyochunguza na kubaini fedha za Chama cha Walimu Tanzania,(CWT) zilivyotumika kwenda kuangalia mpira wa kombe la dunia mwaka 2018.

Manyalika alieleza hayo, wakati akitoa ushahidi katika kesi ya uhujumu uchumi inayowakabili Katibu Mkuu CWT, Deus Seif na mweka hazina wa chama hicho, Abubakar Allawi.

Washtakiwa hao kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka ya matumizi mabaya ya madaraka na kujipatia Sh13.9 milioni mali ya chama hicho.

Akiongozwa na Wakili wa Takukuru, Iman Ntume, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Rashidi Chaungu, shahidi huyo alidai alipokea taarifa za kutumika fedha za CWT, kwenda kuangalia mpira wa miguu Cape Verde mwaka 2018.

Alidai baada ya kupokea taarifa hizo, alianza kuchukua nyaraka mbalimbali za malipo kuhusiana na chama hicho “Nilipata barua ya maombi iliyokuwa na kiasi cha Sh17 milioni ambayo yalipita kwa mshtakiwa wa kwanza Deus Seif, kuidhinishwa na kupelekwa kwa mhasibu afanye malipo,”.

Shahidi huyo wa saba katika kesi hiyo, alidai fedha zilichukuliwa benki na mhasibu aliyetambulika kwa jina la Charles na kukabidhiwa kwa mtu mwingine aliyeitwa Prosper.

“Maelekezo hayo yalitolewa na katibu mkuu ya kufanya malipo, nilipofuatilia benki ya NBC nikaona fedha zilizowekwa zilikuwa zimeandikwa kwa ajili ya kwenda kuangalia mpira na majina yaliyokuwepo ni ya watuhumiwa,” alidai

Shahidi huyo aliendelea kuieleza Mahakama kuwa, baada ya kuomba nakala ya malipo ya posho ya safari kutoka ofisini, mshtakiwa wa kwanza Deus alikataa kuzitoa kwa maandishi akidai ilikuwa ni safari binafsi.

Hata hivyo katika mahojiano na watuhumiwa hao walidai fedha walizotumia zilikuwa za kwao na zilitolewa kwenye akaunti ya NMB. “Pamoja na kukosa muamala wa aina hiyo uliofanyika katika akaunti ya mshtakiwa wa pili Abubakar Allawi, pia alishindwa kuwasilisha vielelezo vya miradi anayodai kufanya ikiwamo ufugaji wa kuku,” alidai shahidi huyo.

Mahakama ilikataa kupokea kielelezo cha upande wa mashtaka, baada ya upande wa utetezi ukiongozwa na Wakili, Nestory Nkoba, kudai zina upungufu wa kisheria. Kesi hiyo imeahirishwa na itatajwa tena Novemba 23, kwa ajili kuendelea na ushahidi wa upande mashtaka.

Chanzo: mwananchidigital