Dar es Salaam. Mbunge wa Kilwa Kusini (CUF), Seleman Bungara ‘bwege’ na viongozi wenzake wawili wamekamilisha taratibu za dhamana na kuachiliwa huru katika Mahakama ya Mkoa wa Lindi.
Viongozi wengine waliachiliwa huru leo Ijumaa Novemba 23, 2018 ni pamoja na Naibu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano kwa umma, Mbarara Maharagande na mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Lindi, Abuu Mjaka.
Wakili anayewatetea washtakiwa hao, Rainery Songea amesema wateja wake walitakiwa watoke jana baada ya kupata dhamana hiyo lakini kukajitokeza hitilafu kwenye barua za wadhamani hali iliyosababisha warudishwe mahabusu.
“Leo kasoro hizo zimerekebishwa na wameachiliwa huru na kesi ya itatajwa tena Desemba 3 mwaka huu,”amesema Wakili Songea.
Viongozi hao walifikishwa jana mahakamani hapo wakikabiliwa na mashtaka ya kutishia, kutoa lugha isiyofaa na kushwawishi watu kufanya makosa.