Dar es Salaam. Mbunge wa Kilwa Kusini (CUF), Seleman Bungara 'Bwege' aliyekuwa anashikiliwa na polisi akidaiwa kutaka kufanya mkutano wa hadhara bila kuwa na kibali ameachiwa huru.
Akizungumza na Mwananchi leo Oktoba 2,2018 Mkurugenzi habari wa CUF, Mbarala Maharagande, amesema kwamba mbunge huyo ameachiwa jana baada ya kukamilisha dhamana.
“Jana hiyohiyo mbona alitoka, kilichokuwa kinatakiwa ni dhamana na tunashukuru kaipata na sasa hivi yuko nje anaendelea na shughuli za kichama’’amesema Maharagande
Mkuu wa Wilaya ya Kilwa Christopher Ngubiagai akizungumza na MCL Digital jana usiku Oktoba 1, 2018 alisema Bwege alikamatwa saa 10 jioni eneo la Maalim Seif lililopo Kilwa Kivinje.
Ngubiagi amesema mbali na Bwege wengine waliokuwa wanashikiliwa na polisi ni madiwani wanne akiwemo diwani wa Kilwa Masoko na mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Abuu Mjaka ambao wote wametoka.
"Bungara alipeleka barua ila kwa sababu za kiusalama polisi walizuia mkutano huo na yeye aliomba asiufanye. Endapo angefanya kungekuwa na uvunjifu wa amani," amesema Ngubiagai ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya hiyo.
Soma zaidi:
Mbunge Bwege ashikiliwa na polisi