Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mashtaka matatu anayedaiwa kumteka Mo Dewji haya hapa

60123 MOO1+PIC

Thu, 30 May 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar Es Salaam. Dereva teksi, Mousa Twaleb (46) amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Jumanne Mei 28, 2019 akikabiliwa na mashtaka matatu likiwemo la kumteka nyara mfanyabiashara Mohamed Dewji ‘Mo’.

Mbali na shtaka la utekaji,  Twaleb  anakabiliwa na shtaka la kutakatisha fedha Sh8milioni pamoja na kujihusisha na genge la  uhalifu.

Twaleb, mkazi wa Tegeta amefikishwa  mahakamani hapo na kusomewa mashtaka yake mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Huruma Shaidi.

Akisoma mashitaka hayo  wakili wa Serikali Mkuu, Paul Kadushi akisaidiana na Wankyo Simon amedai mshtakiwa anakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 42/2019.

Kadushi amedai katika shtaka ya kwanza, mshtakiwa alijihusisha na genge la uhalifu.

Wakili Kadushi amedai  mshtakiwa anadaiwa kutenda kosa hilo kati  ya Mei Mosi, 2018 na Oktoba 10, 2018 katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam na Johannesburg, Afrika Kusini, kwa makusudi alitoa msaada wa kutendeka vitendo vya jinai au uhalifu wa kupangwa kwa lengo la kujipatia faida.

Habari zinazohusiana na hii

Katika shtaka la pili, Twaleb anadaiwa  Oktoba 11, 2018 katika maeneo ya Hoteli ya Colloseum  iliyopo wilayani Kinondoni Dar es Salaam, Twaleb  pamoja na watu wengine ambao hawajafikishwa mahakamani, walimteka nyara Mo kwa nia ya kumhifadhi kwa siri na kumuweka maeneo ambayo ni hatari.

Katika shtaka la tatu, wakili Simon amedai Julai 10, 2018 katika maeneo ya Mbezi Beach wilaya ya  Kinondoni, mshtakiwa alitakatisha fedha Sh8milioni wakati akijua fedha hizo ni kosa la kushiriki genge la uhalifu na makosa ya kupanga.

Mshtakiwa baada ya kusomewa mashtaka yanayomkabili, Hakimu Shaidi amesema  hatakiwi kujibu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo hadi Mahakama Kuu.

Wakili Kadushi amedai kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika, kwamba  wanafuatilia taratibu  za kisheria kwa ajili ya kuwasilisha taarifa Mahakama Kuu.

Hakimu Shaidi baada ya kusikiliza maelezo ya upande wa mashtaka ameahirisha kesi hiyo hadi Juni 11, 2019 itakapotajwa.

Mshtakiwa amerudishwa  rumande kutokana na mashtaka yanayomkabili kutokuwa n dhamana.

Mo alitekwa nyara Oktoba 11, 2018 i katika  maeneo ya Hoteli ya Colloseum alikokwenda kufanya mazoezi na kupatikana Oktoba 20, 2018  katika eneo la Gymkhana.

 

Chanzo: mwananchi.co.tz