Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imekwama kusikiliza ushahidi katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili Yusuf Ali Yusuf maarufu ‘Mpemba wa Magufuli’.
Yusuf na wenzake watano wanakabiliwa na mashtaka manne ikiwemo kujihusisha na biashara haramu ya meno ya tembo yenye thamani ya Sh785.6milioni.
Wakili wa Serikali, Elizabeth Mkude amedai leo Alhamisi Mei 30, 2019 mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba kuwa kesi hiyo imekuja kwa ajili ya kusikilizwa lakini mashahidi wako nje ya Mkoa wa Dar es Salaam na mwingine wagonjwa.
"Kesi imekuja kwa ajili ya kuendelea kusikilizwa lakini mashahidi wapo nje ya Mkoa na mwingine tuliyemtegemea tumeelezwa ni mgonjwa, tunaomba tarehe nyingine,” amedai Mkude.
Hakimu Simba ameeleza kuwa kesi hiyo ni ya muda mrefu tangu 2016 na kitendo cha kutoleta mashahidi hakivumiliki huku akiutaka upande wa mashtaka kuleta shahidi zaidi ya mmoja siku kesi hiyo itakapotajwa tena.
Baada ya maelezo hayo aliahirisha kesi hiyo hadi Juni 13 na 19, 2019 huku washtakiwa wakirudishwa rumande kutokana na mashtaka yanayowakabili kutokuwa na dhamana.
Pia Soma
- UDSM, China kushirikiana kufanya tafiti
- Mwenyekiti UVCCM ataja sababu wagombea CCM kutokubalika
- Dk Abbas asema sekta ya madini Tanzania imeonyesha mwanga
Washtakiwa hao kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka manne, likiwemo la kujihusisha na mtandao wa ujangili katika kesi ya uhujumu uchumi namba 53/2016.
Miongoni mwa shtaka moja kati ya manne yanayowakabili ni kwamba kati ya Januari, 2014 na Oktoba, 2016 katika maeneo ya Jiji la Dar es Salaam, Tanga, Iringa na Mtwara, walijihusisha na mtandao wa ujangili kwa kukusanya na kuuza nyara za Serikali ambazo ni vipande 50 vya meno ya tembo vyenye thamani ya dola za Marekani 180,000 sawa na Sh392,817,600 bila kuwa na kibali cha mkurugenzi wa wanyamapori.