Moshi. Mahakama Kuu Kanda ya Moshi divisheni ya makosa ya uhujumu uchumi imetupilia mbali maombi ya dhamana ya vigogo wa Chama Kikuu cha Ushirika mkoani Kilimanjaro (KNCU) wanaokabiliwa na kosa la uhujumu uchumi.
Washtakiwa hao ni aliyekuwa mwenyekiti wa zamani wa KNCU, Aloyce Kitau; Hatibu Mtanga aliyekuwa makamu mwenyekiti wa zamani wa chama hicho pamoja na Honest Temba ambaye ni meneja mkuu wa KNCU.
Akitoa uamuzi huo leo Ijumaa Agosti 10, 2018 Jaji Wilfrida Koroso amesema mahakama hiyo imepima kwa umakini maombi ya dhamana hiyo na imeona
hayana msingi kwa kuwa suala hilo linagusa maslahi ya wanachama wa KNCU.
Amesema katika hati za viapo vya dhamana
vilivyowasilishwa katika mahakama hiyo ni dhahiri kwamba vilikua si halali kwa kuwa zilionekana zimetolewa kopi, havikuwa halisi.
Amesema tarehe katika hati hizo ni tofauti na tarehe ambayo hati hizo ziliwasilishwa mahakamani hapo huku akifafanua kuwa barua hizo ziliandikwa Agosti Mosi, 2018 na kuwasilishwa mahakamani Agosti 9, 2018.
“Mahakama hii imepima kwa umakini hoja zilizotolewa na mawakili wao upande wa utetezi kuhusu maombi ya dhamana na imeona hayana msingi kwani mahakama lazima iongozwe na misingi ambayo ipo,” amesema.
“Mahakama hii imefungwa na haina cha kufanya kutokana na vifungu vya sheria vinavyotuongoza, hivyo washtakiwa wataendelea kukaa rumande hadi kesi yao ya msingi itakaposikilizwa.”
Vigogo hao wanaokabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi Julai 9, 2018, kwa kutumia madaraka yao vibaya wakiwa viongozi na kukisababishia chama hicho hasara ya Sh2.9.