Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mahakama yatoa maagizo kesi ya Sabaya

3a595993690324ce2702f1cccf1865b5 Mahakama yatoa maagizo kesi ya Sabaya

Tue, 5 Jul 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi imeuagiza upande wa Jamhuri uharakishe upelelezi wa kesi ya aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake wanne na pia upate vibali kuiwezesha kuisikiliza kesi hiyo.

Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama hiyo, Salome Mshasha, alitoa agizo hilo baada ya upande wa utetezi kulalamika kuwa kesi hiyo inacheleweshwa kusikilizwa na wateja wao wanateseka.

Wakili wa Utetezi, Helena Mahuna, aliuomba upande wa Jamhuri uharakishe upataji kibali kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) ili kesi hiyo ianze kusikilizwa.

Aliiambia mahakama kuwa, kesi hiyo imeahirishwa mara ya tatu, huku wateja wao wakiendelea kukaa magereza bila kujua hatima yao na kwamba Sabaya anaumwa.

Awali upande wa mashitaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Kassim Daudi akiwa na Sabikia Mcharo, uliieleza mahakama kuwa upelelezi haujakamilika na hawajapata kibali cha kusikiliza kesi hiyo.

Hakimu Mshasha aliahirisha kesi hiyo hadi Julai 14 mwaka huu. Shitaka la kwanza linawahusu washitakiwa wakidaiwa kuongoza na kushiriki genge la uhalifu katika Wilaya ya Hai Februari 2 mwaka jana.

Katika shitaka la pili, mshitakiwa wa kwanza, Sabaya anadaiwa kuwa Februari 22 mwaka jana aliomba rushwa ya Sh milion 30 kutoka kwa Godbless Swai katika eneo la Bomang’ombe Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro.

Katika shitaka la tatu, Sabaya anadaiwa alijipatia rushwa mil 30 kutoka kwa Elbariki Swai kwa nia ya kuzuia taarifa za uchunguzi zilizohusu ukwepaji wa kodi.

Shitaka la nne na tano liliwakabili washitakiwa wa pili, tatu, nne na tano ambalo ni kumsaidia mshitakiwa namba moja (Sabaya) kushawishi na kujipatia manufaa asiyostahili ya Sh mil 30 kutoka kwa Alex Swai.

Katika shitaka la sita, Sabaya anadaiwa kukiuka maadili ya utumishi akiwa Mkuu wa Wilaya ya Hai na shitaka la saba la utakatishaji fedha linawakabili washitakiwa wote.

Washtakiwa wengine ni Silvester Nyagu, John Aweyo, Nathan Msuya na Antoro Assey.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live