Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mahakama yashindwa kufunga ushahidi kesi ya mauaji ya mwanafunzi shule ya Scolastica

10380 Pic+kesi TanzaniaWeb

Sun, 1 Jul 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Moshi. Mahakama ya Hakimu mkazi mjini Moshi leo Juni 29, 2018 imeshindwa kufunga ushahidi  wa kesi ya mauaji ya mwanafunzi wa Shule ya Scolastica, Humphery Makundi (16) ili kuanza kusikilizwa katika  Mahakama Kuu Kanda ya Moshi kutokana na mkanganyiko wa tarehe ya kutajwa kwa kesi hiyo.

Washtakiwa katika kesi hiyo ya mauaji  ni mmiliki wa shule hiyo, Edward Shayo, mwalimu Labani Nabiswa na mlinzi wa shule hiyo, Hamisi Chacha.

Juni 27, 2018 Hakimu mkazi wa Mahakama ya Moshi, Julieth Mawole aliahirisha kesi hiyo hadi leo kwa ajili ya washtakiwa kusomewa maelezo ya mashahidi na vielelezo vitakavyotumika dhidi yao lakini hawakufikishwa mahakamani kutokana na Magereza kunakili kimakosa tarehe.

 

Kutokana na hali hiyo wakili wa Jamhuri, Agatha Pima ameiomba mahakama hiyo kuahirisha kesi na kupangiwa tarehe nyingine.

 

“Kesi ipangiwe  tarehe nyingine kwani kumetokea tatizo la tarehe, washtakiwa hawakuandikiwa tarehe ya leo, rumande iliandika  tarehe nyingine.  Sisi upande wa Jamhuri tunasisitiza tuko tayari,” amesema.

 

Wakili  anayemtetea mshatakiwa namba mbili, Elikunda Kipoko amesema hajaridhishwa na taarifa hizo na kutaka aelezwe kisa cha washtakiwa hao kutofikishwa mahakamani.

 

Baada ya maelezo hayo, Hakimu Mawole alihoji sababu za washtakiwa kutofikishwa mahakamani licha ya kuwa alipanga kesi hiyo kuendelea leo.

 

Hata hivyo, Mawole ameahirisha kesi hiyo hadi Julai 6, 2018 siku ambayo washtakiwa watasomewa maelezo ya mashahidi na vielelezo  vitakavyotumika dhidi yao kwa ajili ya kufunga ushahidi kwenda Mahakama Kuu.

 

Mwanafunzi huyo anadaiwa kuuawa Novemba mwaka jana na mwili wake kutupwa mita 300 kutoka shuleni hapo na ukazikwa bila kutambuliwa, hadi ulipofukuliwa kwa amri ya Mahakama.

 

 

 

Chanzo: mwananchi.co.tz