Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuachia huru aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Madabida na wenzake watano baada ya Serikali kushindwa kuthibitisha mashtaka dhidi yao likiwemo la kusambaza dawa bandia za kufubaza Virusi vya Ukimwi.
Madabida ambaye pia ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Ltd cha Dar es Salaam (TPI) na wenzake walikuwa wanakabiliwa na mashtaka matano likiwemo ya kusambaza makopo 7,776 ya dawa bandia za kufubaza Virusi vya Ukimwi (ARV) aina ya Antiretroviral, wakijaribu kuonyesha kuwa dawa hizo zilikuwa halali na zimetengenezwa nchini.
Uamuzi huo wa kuwaachia huru umetolewa leo Alhamisi Februari 24, 2022 na Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi wakati kesi hiyo ilipoitwa mahakamani hapo kwa ajili ya uamuzi kama washtakiwa wanakesi ya kujibu au laa.
Mbali na Madabida, washtakiwa wengine ni Mkurugenzi wa Operesheni wa TPI, Seif Shamte, Meneja Masoko, Simon Msofe, Mhasibu Msaidizi, Fatma Shango pamoja na wafanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD), Sadick Materu na Evans Mwemezi.
Hakimu Shaidi amesema upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi 13 na vielelezo zaidi ya 10, lakini umeshindwa kudhibitisha mashtaka dhidi ya washtaka wote, hivyo amewaachia huru washtakiwa wote.