Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mahakama yakubali Malinzi, wenzake kuhojiwa Takukuru

37041 Takukurupic Mahakama yakubali Malinzi, wenzake kuhojiwa Takukuru

Thu, 17 Jan 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Taasisi  ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imeiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutoa kibali cha kumhoji aliyekuwa rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi na  katibu mkuu wa shirikisho hilo, Mwesigwa Selestine.

Wakili wa Takukuru,  Leonard Swai akisaidiana na Nickson Shayo ameiomba Mahakama hiyo leo Jumatano Januari 16, 2019 mbele ya hakimu mkazi mkuu, Wilbard Mashauri wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kuendelea na ushahidi.

Malinzi,  Selestine pamoja na wenzao watatu wanakabiliwa na mashtaka 30 yakiwemo ya kula njama, kughushi na kutakatisha fedha katika kesi ya jinai namba 213/ 2017.

Swai ameieleza mahakama hiyo kuwa wanaomba kibali cha kwenda kuwahoji washtakiwa hao kwa mashtaka mengine tofauti na yanayowakabili Kisutu.

"Tunaiomba Mahakama yako itoe kibali cha kwenda kumhoji mshtakiwa wa kwanza na wa pili katika mashtaka mengine na sio haya yaliyopo mahakama hapa," amedai Swai.

Baada ya maelezo hayo, Hakimu Mashauri alikubaliana na upande wa mashtaka na kuruhusu Malinzi na Selestine kwenda kuhojiwa leo na kurejeshwa Januari 17, 2019.

Baada ya Hakimu kuruhusu washtakiwa hao kwenda kuhojiwa, wakili wa utetezi,  Richard Rweyongeza aliwataja mawakili watakaoambatana na washtakiwa kwenda kuhojiwa Takukuru kuwa ni  Kung'e Wabeya na Adolf Bunyoro.

Hakimu Mashauri ameahirisha kesi hiyo hadi Januari 21, 2019 itakapoendelea na ushahidi.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni mhasibu wa TFF,  Nsiande Mwanga(27), meneja wa ofisi ya TFF, Miriam Zayumba pamoja na Karani wa TFF, Flora Rauya.

Kwa pamoja  wanakabiliwa na mashitaka 30 katika kesi ya jinai namba 213 ya mwaka 2017 yakiwamo ya kula njama, kughushi, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na utakatishaji wa fedha za Marekani 173,335.

Malinzi, Mwesigwa na Nsiande wapo rumande kutokana na  mashtaka ya utakatishaji wa fedha yanayowakabili ambayo hayana dhamana kisheria,  Miriam na Flora wapo nje kwa dhamana.

Tayari mashahidi tisa wa upande wa mashitaka wamekwishatoa ushahidi wao dhidi ya washtakiwa hao.

 



Chanzo: mwananchi.co.tz