Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Madawati ya Ukatili wa kijinsia na Watoto yakaguliwa

ACP Faidha Mratibu wa Dawati la Jinsia na Watoto ACP, Faidha Suleiman

Wed, 27 Apr 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto wametakiwa kushirikiana na Wakaguzi wa Kata pamoja na Maafisa ustawi wa Jamii katika kuzuia makosa ya ukatili wa kijinsia na watoto ili kujenga jamii salama na kizazi chenye kupinga ukatili kwa maendeleo ya taifa.

Hayo yamesemwa na Mratibu wa Dawati la Jinsia na Watoto kutoka Makao Makuu ya Polisi, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Faidha Suleiman wakati wa ziara yake ya ukaguzi wa madawati ya jinsia na watoto katika Mkoa wa Mtwara ambapo aliweza kuzungumza na watendaji wa Dawati, Maafisa Ustawi wa jamii kutoka Manispaa ya Mtawara na Wakaguzi wa Kata kwa lengo la kuboresha utendaji wa madawati hayo.

ACP Faidha amesema uimara wa madawati ya jinsia na watoto katika vituo vya Polisi ni nguzo imara katika kupunguza vitendo vya uhalifu na ushirikiano baina ya watendaji hao ukiimarika utaendeleza juhudi za Serikali katika kupunguza vitendo vya ukatili nchini.

“Kila mmoja ana wajibu wa kuhakikisha anafanya kazi kwa mujibu wa taratibu na kujielekeza kuzuia uhalifu kabla haujatokea hususani kwa kwenda katika mitaa na vijiji ambapo ndipo walipo Wananchi na wahanga wa matukio haya na hili ni jukumu letu sote” Alisema ACP Faidha.

Kwa upande wake Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Nicodemus Katembo amesema wanaendelea na ujenzi wa madawati ya kijinsia na watoto katika vituo vya Polisi kwa mujibu wa taratibu na madawati ambayo tayari yamekamilika wataendelea kuyaboresha ili yaweze kufanya kazi kwa ufanisi.

Alisema uwepo wa Madawati umekuwa ukisaidia siyo kwa Wanawake na watoto pekee bali hata kwa Wanaume ambao kwa sasa wamekuwa wakijitokeza kuripoti vitendo vya ukatili bila woga kutokana na kuwepo kwa Askari maalumu waliopata mafunzo katika kuwasikiliza.

Naye Afisa Ustawi Jamii mkoa wa Mtwara Bi. Theresia Ngonyani alisema wataendelea kushirikiana na Watendaji wa Dawati pamoja na Wadau wengine ili kuhakikisha kuwa lengo la kukomesha vitendo vya ukatili wa kijinsia linafikiwa katika mkoa wa Mtwara.

Mratibu wa Dawati la Jinsia na Watoto kutoka Makao Makuu ya Polisi yupo mkoani Mtwara kwa lengo la kukagua utendaji kazi wa Madawati ya Jinsia na Watoto ambapo tayari ameshakagua Dawati laWilaya ya Mtwata na kituo cha Polisi Nanyamba ambapo pia amefanya vikao na Wadau ili kuhakikisha kuwa madawati hayo yanafanya kazi vyema katika kupunguza vitendo vya ukatili katika jamii.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live