Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

MAUAJI YA MWANAFUNZI WA SCOLASTICA : Mshtakiwa wa kwanza asahau jina la baba mkwe kortini

56034 PIC+SCOLASTICA

Tue, 7 May 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Moshi. Hamis Chacha, mshtakiwa wa kwanza katika kesi ya mauaji ya mwanafunzi Humphrey Makundi, jana alipata wakati mgumu hadi kushindwa kufahamu jina la baba mkwe wake.

Mshtakiwa huyo alijikuta katika wakati mgumu zaidi alipoonyeshwa maelezo aliyoyaandika Novemba 14,2017 shuleni wakati polisi walipofika kuchunguza kupotea kwa mwanafunzi huyo.

Washtakiwa katika kesi hiyo ni Chacha ambaye ni mlinzi wa shule, Edward Shayo mmiliki wa shule akiwa mshtakiwa wa pili na Laban Nabiswa ambaye ni mshtakiwa wa tatu.

Hayo yalijitokeza wakati Wakili wa Serikali mwandamizi, Abdalah Chavulla akimhoji mshtakiwa huyo kutokana na ushahidi wake wa utetezi alioutoa kwa kuongozwa na wakili wake, David Shillatu.

Katika ushahidi wake wa msingi, mshtakiwa huyo alieleza kuwa Novemba 6,2017 ambayo ni siku ambayo mwanafunzi huyo aliuawa, akiwa doria saa 2 usiku alimkurupusha mtu akakimbilia uraiani.

Alidai mara baada ya mtu huyo kukurupuka, alimulika tochi kuona kama kuna watu wengine, lakini hapakuwepo na mtu mwingine eneo hilo na kusisitiza kuwa yeye hakumkimbiza mtu huyo.

Habari zinazohusiana na hii

Baadaye aliieleza mahakama kuwa alimpigia simu mlinzi mwenzake aitwaye Mchamungu Kiwelu, na baadaye akampigia simu Laban na kisha Shayo akiwajulisha juu ya kumkurupusha mtu huyo.

Hata hivyo, wakati akihojiwa jana na Wakili Chavulla aeleze ni maelezo yapi ni sahihi kati ya aliyosema baada ya kumkurupusha hakumkimbiza au alimkimbiza hadi nyumba ya wageni ya BBC.

Sehemu ya mahojiano kati ya shahidi huyo na Wakili Chavulla yalikuwa kama ifuatavyo:

Wakili Chavulla: Nilikusikia hapa ukisema una mke?

Shahidi: Ni kweli mheshimiwa

Wakili Chavulla: Anaitwa nani?

Shahidi: Anaitwa Dorina

Wakili Chavulla: Dorina nani?

Shahidi: Jina la baba yake silifahamu. Ni jina la Kijaluo. Majina ya Kijaluo ni magumu

Wakili Chavulla: Ulimuoa mkeo ukiwa na miaka mingapi?

Shahidi: Sikumbuki ila nilimuoa 2014

Wakili Chavulla: Ulimuoa kimila au ndoa ya Kikristo kanisani?

Shahidi: Ndoa ya kimila

Wakili Chavulla: Unapotaka kuoa ni lazima uwaambie wazazi wako nataka kuoa binti wa fulani, si ndio?

Shahidi: Ndio

Wakili Chavulla: Uliwatajia (wazazi wake) majina ya wazazi wa Dorina?

Shahidi: Mie niliwaambia nataka kuoa

Wakili Chavulla: Jina la baba mkwe wako unalisahau kwa sababu ni gumu, ndivyo unavyotaka mahakama iamini hivyo?

Shahidi: Kweli silikumbuki ni jina gumu

Wakili Chavulla: Namba ya mke wako ni ngapi?

Shahidi: Yeye simu yake ilichukuliwa na mtoto wake akawa anatumia simu ya mdogo wake?

Wakili Chavulla: Ni namba ngapi hiyo simu ya mdogo wake?

Shahidi: Siikumbuki ila inaanza na 0716 na kuishia na 22

Baada ya kueleza hivyo, Wakili Chavulla aliomba apatiwe kielelezo namba 7 cha mahakama ambayo ni taarifa ya mawasiliano ya simu ya washtakiwa waliyoyafanya usiku wa Novemba 6,2017.

Katika kielelezo hicho, shahidi huyo aliitaja namba ya mkewe na kueleza kuwa siku ya tukio alimpigia simu saa 2:57 usiku na kusisitiza kutokana na upendo huwa wanawasiliana mara kwa mara.

Wakili Chavulla: Unamfahamu mshtakiwa wa tatu (Laban)?

Shahidi: Ndio ni Mwalimu Laban

Wakili Chavulla: Mwalimu Laban anamfahamu mkeo?

Shahidi: Hapana hamfahamu

Wakili Chavulla: Mwalimu Laban ana mawasiliano na mkeo?

Wakili Chavulla: Mimi nakuambia mwenye hiyo namba unayodai ni mkeo anamjua Laban?

Shahidi: Sio kweli

Wakili Chavulla akampa tena kielelezo namba 7 na kumtaka aeleze namba hiyo kama iliwasiliana na Laban na baada ya kusoma ilionyesha Laban aliwasiliana na mwenye namba hiyo zaidi ya mara nne.

Wakili Chavulla: Hebu iangalie hii nyaraka (akampa) utuambie kuanzia tarehe 7.11.2017 hadi 13.11.2017 ni wakati gani uliwasiliana na huyo mke wako?

Shahidi: Sikuweza kuwasiliana naye tena.

Wakili Chavulla: Sasa nakuambia mwalimu Laban alikuwa anawasiliana na mkeo, lakini wewe mwenye mke hujawasiliana naye kwa siku zote hizo, ndio unataka mahakama iamini hivyo?

Shahidi: Mimi siwezi kujua kama wanawasiliana

Wakili Chavulla: Nakuambia wewe ni mwongo. Nikikuambia mwenye hiyo namba sio mke wako bali mwenye namba hiyo anaitwa Justine Eliezer na yuko Himo na biashara zake zinajulikana.

Shahidi: Siwezi kujua alitumia kitambulisho gani kusajili.

Mwanafunzi Humphrey Makundi (16), aliyekuwa akisoma kidato cha pili anadaiwa kuuawa usiku wa Novemba 6,2017 na mwili wake kutupwa katika Mto Ghona uliopo mita 300 kutoka shuleni hapo.

Kesi hiyo itaendelea leo



Chanzo: mwananchi.co.tz