Dar es Salaam. Mfanyabiashara na mkazi wa Mlandizi mkoani Pwani nchini Tanzania, Mohammed Simon (29) amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, akikabiliwa na shtaka la kusafirisha dawa za kulevya aina ya Mirungi kilo 447.89.
Simon alifikishwa mahakamani hapo jana Ijumaa Agosti 9, 2019 na kusomewa shtaka lake, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa mahakama hiyo, Janeth Mtega.
Wakili wa Serikali, Nancy Mushumbusi alidai mshtakiwa huyo anakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi.
Mushumbusi alidai mshtakiwa anadaiwa kutenda kosa hilo, Julai 29, 2019, katika la eneo la Posta Mpya.
Mshatakiwa huyo anadaiwa siku hiyo na eneo hilo, alikuwa akisafirisha mirungi kilo 447.89, wakati akijua kuwa ni kosa kisheria.
Mshtakiwa hakutakiwa kusema chochote kutokana na shtaka linalomkabili kutokuwa na dhamana.
Pia Soma
- TBPL ilivyojipanga kutokomeza malaria, yapata soko SADC
- Masauni atoa miezi miwili kwa madereva
- MCL yafafanua taarifa za madai ya mfanyakazi wake kuhusika na dawa za kulevya
Katika hatua nyingine, wafanyabiashara wawili wa Tabata, Dar es Salaam, Salaam Mahamud (21) na Jabiri Othmani (27), wamepandishwa mahakamani hapo wakikabiliwa na shtaka la kusafirisha dawa za kulevya.
Washtakiwa hao wanadaiwa kusafirisha dawa za kulevya aina ya Mirungi kilo 84.4, kinyume cha sheria.
Mahamud na Othman wanadaiwa kutenda kosa Agost 7, 2019 katika maeneo tofauti ya jijini Dar es salaam.