Mkazi wa Magomeni, Simon Yagaza (24), amefikishwa katika Mahakama ya Mwanzo Kariakoo, kujibu shtaka la kujipatia Sh801,600, kwa njia ya udanganyifu.
Yagaza anadaiwa kuaminiwa na kikundi na kukopesha kiasi hicho cha fedha, lakini muda wa kulipa mkopo huo ulipofika alitoweka.
Mshtakiwa huyo amefikishwa mahakamani hapo leo, Desemba 10, 2023 na kusomewa shtaka lake na Karani, Caroline Nyonyi.
Karani Nyonyi alidai mshtakiwa alitenda kosa hilo Oktoba 23, 2023 eneo la Kisutu, Wilaya ya Ilala.
Alidai mbele ya Hakimu Gladness Njau, kuwa siku ya tukio, kwa kuaminiwa na wanakikundi kupitia Kampuni ya Suprime alipatiwa mkopo wa Sh801,600 na baada ya kupata mkopo huo mshtakiwa alitoweka na fedha hizo, hadi alipokamatwa.
Yagaza baada ya kusomewa shtaka hilo alikana kutenda kosa hilo na kuomba apewe dhamana.
Hakimu Njau, alitoa masharti ya dhamana ambapo mshtakiwa huyo analitakiwa kuwa na wadhamini wawili wenye barua za utambulisho watakaotia saini dhamana Sh300,000 kila mdhamini.
Mshtakiwa ameshindwa kutimiza masharti ya dhamana hivyo alirudishwa mahabusu hadi Desemba 19, 2023 kesi hiyo itakapoitwa kwa ajili ya kutajwa na upelelezi bado haujakamilika.