Serengeti. Wakazi wawili wa kijiji cha Bonchugu wilayani Serengeti wamefikishwa mahakamani kwa makosa ya kukutwa na mzoga wa mnyamapori aina ya pongo mwenye thamani ya Sh1.3 milioni.
Mbele ya Hakimu mkazi mfawidhi wilaya ya Serengeti, Ismael Ngaile, mwendesha mashitaka wa Serikali, Emmanuel Zumba amewataja washitakiwa kuwa ni Weisiko Mgesi (29) na Makuri Marwa(25).
Amesema kwa pamoja washtakiwa hao wanatuhumiwa kwa makosa matatu ya uhujumu uchumi.
Katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 115/2018 amesema kosa la kwanza ni kuingia ndani ya hifadhi, la pili kupatikana na silaha za jadi ndani ya hifadhi na la tatu ni kupatikana na nyara za Serikali bila kibali.
Amesema kwa pamoja walikamatwa Oktoba 18, 2018 katika eneo la Risiliba ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Washitakiwa hawakutakiwa kujibu chochote na kesi imeahirishwa hadi Novemba 2, 2018 na wamepelekwa mahabusu.