Dar es Salaam. Geogre Mwamgabe (44), ofisa usalama wa Shirika la Posta Tanzania na dereva wa shirika hilo, Abrahamani Msimu wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na kosa la kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin gramu 1.55 na bangi gramu 124.55.
Akisoma hati ya mashtaka leo Jumatano Oktoba 2, 2019 mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Augustina Mbando wakili wa Serikali, Adolf Lema amedai Agosti 25, 2019 makao makuu ya shirika hilo Ilala jijini Dar es Salaam, washtakiwa walisafirisha bangi.
Katika shtaka la pili wanadaiwa kuwa Agosti 25, 2018 jijini Dar es Salaam walisafirisha Heroin.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo washtakiwa hao walikana kufanya makosa hayo.
Hakimu Mmbando amesema dhamana ipo wazi lakini washtakiwa walishindwa kutimiza masharti na kurudishwa rumande hadi Oktoba 16, 2019.