Dar es Salaam. Upelelezi wa kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili aliyekuwa mkurugenzi wa Kampuni ya Usafiri wa Mabasi yaendayo Kasi (Udart), Robert Kisena na wenzake akiwemo mkewe, Florencia Mashauri bado haujakamilika.
Hayo yameelezwa leo Jumanne Juni 11, 2019 na wakili wa Serikali, Ester Martin mbele ya hakimu mkazi mwandamizi, Augustine Rwizile wakati shauri hilo lilipofikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa.
Hakimu Rwizile baada ya kusikiliza maelezo ya upande wa mashtaka, aliahirisha kesi hiyo hadi Juni 24, 2019 itakapotajwa tena huku washtakiwa wakirudishwa rumande kutokana na mashtaka yanayowakabili kutokuwa na dhamana.
Mbali na Kisena, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 38/2019 ni Kulwa Kisena, raia wa China Chen Shi na mhasibu wa kampuni hiyo, Charles Selemani.
Washtakiwa kwa pamoja wakabiliwa na mashtaka 19, yakiwemo ya utakatishaji fedha na kuisababishia Udart hasara ya Sh2 bilioni.