Dar ss Salaam. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), imetuma maombi nje ya nchi kwa ajili ya kufanya upelelezi katika kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili, aliyekuwa mkurugenzi wa mipango na ufuatiliaji na tathmini wa Taasisi hiyo, Kulthum Mansoor.
Mansoor anakabiliwa na makosa nane likiwemo la utakatishaji fedha kiasi cha Sh1.4 bilion, katika kesi ya uhujumu uchumi, iliyopo mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Wakili wa Takukuru, Maghela Ndimbo ameieleza Mahakama hiyo leo Jumanne, Juni 4, 2019, mbele ya Hakimu Mfawidhi, Kelvin Mhina.
Ndimbo amedia kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya kutajwa na kwamba upelelezi wake bado haujakamilika.
"Tumetuma maombi nje ya nchi kwa ajili ya kukamilisha upelelezi katika nchi hizo, hivyo tunasubiri majibu kuhusiana na maombi hayo," amedai Ndimbo.
Ndimbo baada ya kueleza hayo, Hakimu Mhina ameahirisha kesi hiyo hadi Juni 18, 2019 itakapotajwa na mshtakiwa amerudishwa rumande kutokana na mashtaka yanayomkabili kutokuwa na dhamana.
Pia Soma
- RC Mtwara azindua soko la madini
- SIKUKUU YA EID: Wafanyabiashara, wananchi wapongezana bei za bidhaa
- Mwalimu akamatwa na silaha ya kivita, nyara za Serikali
Kuanzia shtaka la pili hadi la saba, anadaiwa, kati ya Januari 2012 na Mei 2017 akiwa eneo la Upanga, mshtakiwa alijipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kiasi cha Sh1.477,243,000 kutoka kwa watumishi sita wa Takukuru, kama malipo ya viwanja vilichopo kijiji cha Ukuni wilayani Bagamoyo huku akionyesha yeye ni mmiliki, jambo ambalo alijua ni uongo.
Katika kosa la nane, ambalo ni la kutakatisha fedha, mshtakiwa anadaiwa kati ya 2013 na Mei 2018 akiwa eneo la Upanga jijini Dar es Salaam, alijipatia kiasi hicho cha fedha huku akijua fedha hizo ni zao la makosa mengine.