Dar es Salaam. Upande wa mashtaka katika kesi ya kukutwa na dawa za kulevya inayomkabili, Abdul Nsembo maarufu Abdulkandida (45) na mkewe, Shamim Mwasha (41) umeieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa wanasubiri majibu ya kielelezo kilichopelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kwa ajili ya uchunguzi.
Nsembo na Shamimu wakabiliwa na shtaka moja la kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroini, kinyume cha sheria, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu,
Wakili wa Serikali Jenifer Massue, ameeleza hayo leo Jumatatu, Juni 10, 2019, wakati kesi hiyo ilipofikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa.
Massue ameeleza hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Kelvin Mhina.
"Upande wa mashtaka kwa sasa tunasubiri majibu ya kielelezo kilichopelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kwa ajili ya uchunguzi" Alidai Wakili Massue.
Massue amedai kuwa kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya kutajwa na upelelezi wake bado haujakamilika, hivyo wanaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.
Pia Soma
- Ofisa wa TRA na askari polisi, kortin kwa kuomba rushwa ya Sh2 milioni
- LIVE: MAGUFULI AKIWAAPISHA VIONGOZI NA KUPOKEA GAWIO KUTOKA KAMPUNI YA BHARTI AIRTEL IKULU DAR
- Hospitali ya Aga Khani yatangaza neema kwa wanawake, watoto Tanzania
- Muswada kila bodaboda kuwa na bima ya afya wanukia
Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 36/2019.
Katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 36/2019, washtakiwa kwa pamoja wanadaiwa kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroini zenye uzito wa gram 232.70, wakati wakijua kufanya hivyo ni kosa kisheria.
Wanadaiwa kutenda kosa hilo, Mei mosi, 2019 katika eneo la Mbezi Beach, Jijini Dar Es Salaam.
Kwa mara ya kwanza, washtakiwa hao walifikishwa Kisutu, Mei 13, 2019.