Dar es Salaam. Hamisi Saidi (38) ‘Meshack’ ambaye ni mfanyabiashara na Mkazi wa Gezaulole wilaya ya Kigamboni, Dar es Salaam amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akituhumiwa kumuua mke wake Naomi Marijani.
Akisoma hati ya mashitaka leo Jumanne Julai 30, 2019 Wakili wa Serikali, Wankyo Simon mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Ally Salum amedai mshitakiwa huyo anashitakiwa kwa kosa la mauaji kifungu cha 196 cha kanuni ya adhabu sura ya 16 kilichofanyiwa marejeo mwaka 2002.
Simon amedai Mei 15, 2019 eneo la Gezaulole wilayani Kigamboni alimuua Naomi Marijani huku akijua kufanya hivyo ni kosa la kisheria.
Amedai bado wanaendelea na upelelezi hivyo anaiomba Mahakama hiyo ipange tarehe nyingine ya kutajwa shauri hilo.
Hakimu Salum amesema Mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo hivyo mshtakiwa huruhusiwi kujibu chochote.
Ally ameahirisha shauri hilo hadi Agosti 13, 2019 itakapo tajwa tena.