POLISI mkoani Morogoro wamemkamata mtu aliyetambuliwa kwa jina la Isihaka Exavery (20) mkazi wa Mkundi, manispaa ya Morogoro kwa tuhuma za kuchana picha za mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), John Magufuli.
Kijana huyo pia anatuhumiwa kuchana picha za mgombea udiwani kata ya Mkundi kupitia CCM .
Kamanda wa Polisi wa mkoa huo Wilbroad Mutafungwa, alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea Oktoba 15 mwaka huu saa tano asubuhi katika mtaa wa Mlimani, kata ya Mkundi, Manispaa ya Morogoro.
Kamanda Mutafungwa alisema kijana huyo alichana picha za Magufuli na za ombea Seif Zahoro Chomoka, akakimbia.
Alisema, Polisi baada ya kupata taarifa hizo walifika eneo la tukio na kuanza msako na kwa kushirikiana na wananchi walioshuhudia tukio hilo walimkamata mtuhumiwa huyo na picha alizochana.
Kamanda Mutafungwa alisema Polisi wanaendelea kumhoji kijana huyo na kwamba upepelezi ukikamilika atafikishwa mahakamani.