JESHI la Polisi Mkoa wa Temeke limemkamata mkazi wa Mbande Rufu, Aziz Abdallah (39) akiwa na magunia 31 yaliyojaa bangi akiwa ameyahifadhi ndani ya nyumba anayoishi.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa mkoa huo wa Kipolisi, Amon Kakwale, Abdallah alikamatwa Februari 12 mwaka huu saa 12 asubuhi katika eneo la Mbande Rufu wilayani Temeke.
Kamanda Kakwale alisema, mtuhumiwa huyo pia alikutwa na Sh milioni mbili zinazodaiwa kutokana na mauzo ya bangi aliyoiingiza Dar es Salaam kwa kutumia lori kutoka Morogoro.
"Kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo kumetokana na operesheni mbalimbali inayoendelea kufanywa na jeshi letu na kumbaini mtuhumiwa kujishughulisha na biashara hiyo haramu" alisema.
Kamanda Kakwale alisema, baada ya Polisi kupokea taarifa kutoka kwa wasamaria wema walifika katika nyumba ya mtuhumiwa huyo na kuanza kupekua na ndipo walipobaini kuwepo kwa bangiyo.
Alisema baada ya upekuzi huyo, walibahatika kukuta maguni 24 yaliyojaa, magunia 14 yalikuwa na bangi nusu gunia kila moja hivyo ni sawa na magunia saba yaliyojaa, na madebe matatu yaliyojaa mbegu za bangi.