Nairobi. Mmiliki wa ghala ambalo imekutwa sukari iliyoingizwa kwa magendo nchini Kenya anashikiliwa na polisi.
Jumapili iliyopita mkuu wa polisi wa Kitui Muthuri Mwongera alisema kwamba mmiliki huyo atafikishwa mahakamani leo.
Amesema kwamba wamejiridhisha kwa kuangalia vielelezo vya mmiliki huyo kuhusu uingizaji wa sukari hiyo nchini humo.
Mfanyabiashara huyo anashikiliwa tangu Ijumaa huku ghala hilo likiwa limefungwa baada ya kukutwa na mifuko mingi ya sukari hiyo ya magendo.
Kamanda Mwongera amesema kwamba wamechukua sampuli na kuipeleka kwa mkemia mkuu kwa ajili ya uchunguzi ili kujua ni kwa nini haikulipiwa kodi.
Ofisa wa Mamlaka ya Mapato Kenya (KRA) Mburu Githii amesema kwamba akiwa na timu yake walichunguza sukari hiyo kwa kuchukua sampuli kwenye maduka yaliyopo maeneo ya Kitui, Matuu na Mwingi.
“Uchunguzi umebaini kwamba sukari hiyo haikulipiwa kodi, na inaonekana ina sumu lakini tunasubiri uchunguzi wa mkemia mkuu wa Serikali,’’amesema ofisa huyo
Naye Gavana wa Kitui Charity Ngilu ameonya wafanyabiashara wanaouza sukari hiyo.